Featured Posts

Saturday, June 14, 2014

Breaking news: Bomu laua mmoja na kujeruhi kadhaa Zanzibar usiku huu (TAHADHARI YA PICHA ZA KUTISHA)

Tunaomba radhi kwa picha hizi ambazo ni graphic. Tumejitahidi kuficha sura ya marehemu
Mwili wa mtu aliyeuawa kutokana na shambulio hilo la bomu

Mtu mmoja ameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa katika shambulio la bomu karibu na msikiti huko Zanzibar. Kwa mujibu wa polisi, shambulio hilo lilitokea katika eneo la Stone Town kwenye sehemu ya biashara ya Darajani.

Mashuhuda wa tukio hilo walieleza kwamba miongoni mwa majeruhi ni waumini waliokuwa wanatoka kuswali katika msikiti ulio jirani na eneo hilo.

"Tunafanya uchunguzi kutambua aina ya bomu, waliohusika na shambulio hilo na lengo lao. Tunaomba wananchi kutupatia taarifa," alisema afisa mwandamizi wa jeshi la Polisi, Mkadam Khamisi.

Taarifa zaidi kuhusu tukio hili la kusikitisha zitawajia kadri zinavyopatikana

Thursday, June 12, 2014

Habari na picha: Huku nchi ikiwa taabani kifedha, angalia matumizi haya ya vigogo wa juu CCM

Wakati taarifa zinatanabaisha kuwa nchi yetu ipo hoi kifedha,

Embedded image permalink

 huku deni la taifa likizidi kupaa, na serikali ikikuna kichwa kutengeneza bajeti ya kueleweka kwa mwaka ujao wa fedha, 

Embedded image permalink
haya ndio matumizi ya viongozi wajuu wa chama Tawala CCM



CHANZO: Jamii Forums

Nakuachia wewe msomaji na kila anayeipenda Tanzania kwa dhati kutoa hukumu hapo mwakani katika uchaguzi mkuu.

Saturday, May 31, 2014

Usiteseke kimyakimya peke yako: Soma mfano hai wa watu wanakuandama mtandaoni bila sababu (TROLLS)

Licha ya kuwa sehemu muhimu za kubailishana mawazo, na pengine kufahamiana na watu mbalimbali, mitandao ya kijamii (social networks) ina upande wa pili ambao kwa hakika unaweza kuyafanya maisha yako yawe magumu mtandaoni. Pengine umeshawahi kusikia kuhusu watu wanaoitwa TROLLS. Pengine ushawahi kukutana nao, iwe Twitter au Facebook au hata Instagram. TROLL ni mtu anayeamua kukuandama kwenye mtandao wa kijamii pasipo sababu ya msingi.

Mara nyingi TROLLS humwandama mtu mwenye umaarufu bila kujali umaarufu huo unatokana na nini. Mtandao wa kijamii unaopendelewa zaidi na TROLLS ni Twitter. Na mara nyingi TROLLS humwandama mtu mwenye followers wengi, pengine lengo likiwa ni kusababisha madhara makubwa kwa mtu huyo. Hapa ninamaanisha kuwa kwa mfano TROLL anapo-tweet kitu kibaya dhidi yako, anatamani watu wengi wakione. Sasa ukiwa na followers wengi, lengo la TROLLS kukudhalilisha linafanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani kila follower wako ataona kitu hicho.

Kuna wanaotetea tabia hiyo chafu wakidai kuwa ni sehemu tu ya utani huku wengine wakidai ni uhuru wa kuongea (freedom of speech). Lakini ukweli ni kwamba TROLLS husukumwa na kauli za chuki (hate speech). Katika mazingira ya kawaida tu, mtu anayekudhalilisha hadharani anakuwa na lengo moja tu: kukudhalilisha. Ndio, uhuru wa kujieleza (freedom of expression/speech) ni kitu kizuri lakini sote twafahamu kuwa hakuna uhuru bila wajibu. Huwezi kumwandama au kumdalilisha mtu hadharani kisha ukajitetea kuwa unatumia uhuru wako wa kujieleza. Uhuru wa kujieleza shurti uambatane na wajibu wa kutowabughudhi watu wengine.

Jana nimekumbana na TROLL mmoja huko Twitter. Huyu jamaa tulikuwa tunaelewana kitambo. Sio marafiki as such lakini mara nyingi tulikuwa tukijadialana kuhusu masuala mbalimbali. Yeye ni mwana-CCM, kwa maana ya kuisapoti CCM,ilhali mie sio kama ni mpinzani wa chama hicho tawala bali ninapinga matendo mengi yasiyopendeza, hususan ufisadi. Kwahiyo mara kadhaa mie na huyu ndugu tulikuwa tukijikuta katika malumbano ya hoja, japo mara zote yalikuwa ya kistaarabu.

Siku moja nikabaini kuwa ameni-unfollow. Nikiri kwamba nilishtushwa na uamuzi wake huo kwa sababu sikuwa na uhasama nae, na hata siku moja sikuwahi kutamka neno baya dhidi yake. Hata hivyo, niliheshimu uamuzi wake huo hasa ikizingatiwa kuwa awali ni yeye ndiye aliyeanza kuni-follow na mie nikam-follow back. Kwa maana hiyo, kama nafsi yake ilivyomtuma kuni-follow mwanzoni, niliamini kuwa nafsi yake hiyohiyo ndiyo iliyomtuma kuni-unfollow.Ila kwa hakika uamuzi wake huo wa kuni-unfollow pasi sababu ulinishangaza.

Nirejee tukio la jana. Hapa chini ndio tweet niliyoifahamu uwepo wake kupitia kwa dadangu yangu mmoja aliyenijulisha kwa Whatsapp, 


Huhitaji kuwa muelewa wa kauli za kashfa kutambua kuwa lengo la mtu huyu halikuwa jema. Ila kukuweka mahala pazuri kuelewa anachoongelea, ni vema nikiambatanisha maelezo na picha ya 'event' (tukio) anayoongelea. Jumatano ya tarehe 28 mwezi huu, nilialikwa jijini London kutoa mada katika semina kuhusu Rushwa na Haki za Binadamu nchini Tanzania. Semina hiyo iliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Kundi la Wanasheria wa Kimataifa wa Haki za Binadamu (Solicitors International Human Rights Group) na Taasisi za Stadi za Juu za Sheria (Society for Advanced Legal Studies). Semina hiyo ilifanyika Institute of Legal Studies ya Chuo Kikuu cha London (University of London)

Pengine kutokana na kutokuwa na uelewa wa events zinazoendeshwa kitaasisi, mtu huyo alitamani kuona picha zangu nyingi nikiwa katika tukio hilo ili kuthibitisha kuwa kweli nilihudhuria na kutoa mada. Lakini licha ya ukweli kwamba sikwenda kwenye tukio hilo kwa ajili ya kupiga picha, pia mie kama mtoa mada ningeonekana kituko kuwa busy na kujipiga picha badala ya kutekeleza jukumu lililonipeleka hapo. Vilevile, yeyote anayeyafahamu vema maisha yangu mtandaoni atatambua kuwa sina tabia ya kujipiga picha, na kwa hakika picha zangu binafsi ni chache mno mtandaoni. Nina sababu zangu za msingi kutotaka kuweka picha zangu mtandaoni, na hilo ni suala binafsi.

Lakini hata tukiweka kando sababu nilizotoa hapo juu, mtu huyu ambaye awali alini-unfollow alikuwa anahitaji nini katika picha zangu? Je akishaziona zitamsaidia nini yeye? Na ukiangalia hiyo tweet yake utabaini ameweka inverted comas kwenye 'usalama wa taifa' kana kwamba mtajwa (mie) ninatumia ndivyo sivyo uhusiano wangu na taasisi hiyo. Sijawahi kuficha kuwa niliwahi kuwa mtumishi wa taasisi hiyo, lakini hilo ni suala langu binafsi ambalo sidhani kama linahitaji kumnyima raha mtu mwingine. Kuwa shushushu sio dhambi, na kwa hakika ninajivunia utumishi wangu katika taasisi hiyo kwa miaka kadhaa, sio kwa sababu ya 'ujiko' bali ukweli kwamba taaluma ya intelijensia inahusiana na kiwango cha juu kabisa cha akili (intelligence) na uzalendo. 

Kilichonisikitisha zaidi katika tukio hilo ni mtu mwingine aliyekuwa anani-follow na mie ninam-follow kuamua ku-RT (retweet) tweet hiyo ya kebehi. Huyu jamaa aliye-RT tuna historia ndefu kidogo. Awali tulikuwa 'marafiki' katika Twitter, ikatokea tukatibuana, nikam-block, lakini katika kuukaribisha mwaka mpya mmoja (nadhani mwaka juzi) alinisihi tusahau tofauti zetu na tuishi mtandaoni kwa amani. Nikam-unblock, na tukaendeleza 'urafiki' wetu huko Twitter. Nilitarajia kuwa kama 'rafiki' angetambua wazi dhamira ya mtu aliye-tweet kuhusu ushiriki wangu katika event hiyo ya London. Na kwa vile ninaamini ni mwelewa, angebaini pia kuwa kui-RT tweet hiyo sio tu kuna lengo la kunifikishia ujumbe bali pia ni kama ana lengo la kuisambaza tweet hiyo ninayoitafsiri kuwa ya kashfa (offensive/malicious)..

Ilinisikitisha kwa sababu kama nilivyoeleza awali, huyu ndugu tulikuwa marafiki, tukatibuana, nikam-block kwa sababu kama hii aliyotenda jana, akataka suluhu,nikaafikiana nae, lakini cha ajabu karejea hukohuko alikotoka. Huu si uungwana hata kidogo na ndio maana nimem-block tena, safari hile milele daima.

Huu ni mfano hai wa TROLLS, watu wanaoamua kukuandama pasi sababu ya msingi. Lakini tafiti mbalimbali zinabainisha kuwa wengi wa TROLLS ni watu wenye matatizo ya kiakili. Hawa ni watu wanaokerwa kuona mtu flani anakubalika kwa jamii (angalau katika mawazo yao), au anapiga hatua flani (na pengine si hatua bali mtizamo wao fyongo tu), au anapata sifa (na pengine sio sifa bali ni sehemu ya kawaida tu ya maisha ya mtu). Ni viumbe wanaosukumwa na chuki, watu wasiopenda kuona flani ana amani. Ni magaidi wa mtandaoni wanaosukuwa na chuki. Ni watu waliokosa kitu flani lakini wanataka kufidia pengo la walichokosa kwa kumwandama mtu aliyenacho. Kwa mfano, chuki ya TROLL yaweza kusababishwa na uhaba wa elimu na hivyo kuwaandama watu walioelimika dhidi yake.

Nieleze bayana kuwa sihitaji kuweka ushahidi wa nifanyacho maishani mwangu, iwe ni kuhudhuria semina, kutoa mada katika semina au jinsi ninavyoishi. Ninaamini kuwa masuala binafsi yanapaswa kubaki binafsi (private things should remain private). Sababu kubwa ya kutopendelea kubandika picha zangu mtandaoni ni hiyo. Sipendi kuyaweka maisha yangu binafsi hadharani. 

Lakini hata kama kulikuwa na umuhimu wa picha za tukio hilo kuwa hadharani (na taasisi husika itaziweka kwenye tovuti yake), kulikuwa na haja gani ya mtu au watu kutaka ushahidi wa picha hizo? Halafu kuna namna ya kistaarabu ya kutaka ushahidi badala ya kukimbilia kuhisi kuwa  "event ilibuma (haikufanikiwa, ni kitchen party..." na kushauri kui-Adobe (akimaanisha kutengenza picha feki za tukio hilo.

Binafsi sikumbuki idadi ya seminars, conferences,workshops na mikusanyiko mingine ambayo nimeshawahi kuhudhuria maishani. Ni mingi mno lakini cha muhimu sio idadi ya misanyiko ya aina hiyo bali umuhimu wake kwangu bainfsi na kwa jamii. Semina hiyo ya London ilikuwa na umuhimu mkubwa kwangu binafsi na kwa Watanzania kwa ujumla, kwa sababu mie binafsi nimekuwa nikijihusisha na vita dhidi ya rushwa na pia rushwa na ukiukwaji wa haki za binadamu ni matatizo sugu huko nyumbani.

Hivi kweli serioulsy mtu anaweza kushauri kutengeneza picha feki kwa Adobe ili kuidanganya jamii kuhusu ushiriki wake kwenye tukio flani? Ili iweje na imsaidie nani? Ama kwa hakika shule ni kitu muhimu sana. Kuna wenzetu wanaishi kwa SIFA na wanahangaika kusaka SIFA kwa gharama yoyote ile. Na kwa hakika, wakipata fursa kama hiyo niloipata juzi basi wangemwaga mapicha lukuki ya kila dakika ya uwepo wao hapo. 

Kama nilivyosema awali, kilichonipeleka katika semina hiyo ni umuhimu wake kwangu na kwa nchi yangu kwa ujumla. Kamwe sijawahi kufanya jambo kwa minajili ya kusaka sifa au maonyesho. Nilizaliwa na kukulia katika kile Waingereza wanakiita humble background. Na ukubwani, nikapata ajira inayohitaji 'maisha ya kificho' kwa aina flani. Simlazimishi mtu kunitafsiri tofauti, kwa sababu siishi kwa kumridhisha mtu flani bali Mola wangu pekee.

Mwisho, ni vema kwa mtu huyo kutambua madhara ya TROLLING. Pengine kwa huko nyumbani ni jambo la kawaida kumsambulia mtu mtandaoni pasi sababu lakini kwa wenye uelewa wa sheria za mtandaoni wanafahamu athari za kudhani ukiwa kwenye keyboard ya kompyuta yako una uhuru wa kuandika chochote kile hata kama kina madhara ya kisheria. Ukweli kwamba hakuna Mtanzania hata mmoja aliyewahi kuchukuliwa hatua za kisheria kwa 'kashfa mtandaoni' sio sababu ya kumwaminisha mtu kuwa kashfa mtandaoni sio kosa kisheria. Japo sitamani kuwa Mtanzania wa kwanza kumchukulia hatua za kisheria mtu anayenikashifu mtandaoni, lakini pindi ikibidi nitafanya hivyo ili iwe fundisho kwa kila anayedhani TROLLING ni ruksa kwa Watanzania.

Mwisho kabisa ni wito wangu kwa Watanzania wenzangu hasa mtandaoni. Tusikatishane tamaa kwa sababu ya chuki binafsi. Kama mtu anajituma kufanya jambo flani iwe lake binafsi au kwa maslahi ya taifa lake basi kama haiwezekani kumsapoti basi ni vema kukaa kimya tu. Kwanini ukerwe na jambo lisilokuhusu? Ni matumaini yangu kuwa waraka huu utasaidia sio tu kupunguza chuki zisizo na msingi mtandaoni bali utasaidia kuhamasisha mapambano dhidi ya TROLLS. Kamwe usiumie kimyakimya mtu anapokubughudhi mtandaoni, maana hicho ndicho kinachowapa nguvu TROLLS-kukuona unateseka kimyakimya. Ni muhimu kukabiliana nao hata kama silaha yao kuu ni kashfa na matusi. Kuna sheria kali tu dhidi ya watu wa aina hiyo, na ikibidi ni muhimu kujikinga au kutafuta haki kwa kutumia sheria hizo.

Pia napenda kuwashukuru TROLLS hao wawili, aliyepost tweet ya kejeli na huyo aliye-RT. Japo kitendo chao kimenisikitisha lakini kwa upande mwingine kimenihamasisha. You see, kama kuna mtu anakerwa na jambo zuri unalofanya kwa ajili yako au kwa ajili ya jamii, njia bora ya kumdhibiti sio kuacha jambo hilo bali kuliendeleza zaidi. Labda siku moja atachoka kuwa hater, au pengine atakufa kwa presha kutokana na mwendelezo wako katika jambo hilo.

I hope ujumbe umefika kwa wahusika, na samahani kwa waraka huu mrefu.

PEACE AND LOVE 

Friday, April 25, 2014

Makala yangu ya RAIA MWEMA Toleo la 23.04.14: "Wazimu Huu wa Udini ni Hatari" #KatibaMpya

NI dhahiri sasa kuwa mjadala wa Katiba mpya, hususan kipengele cha muundo wa Muungano, unaelekea kulipeleka taifa mahali pabaya. Japokuwa dalili za Bunge Maalumu la Katiba linaweza kuishia kuwa jukumu ghali kwa walipakodi masikini, hasa baada ya kusikika madai ya baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo kuwa posho ya shilingi 300,000 kwa siku haitoshi, lakini Watanzania wengi walikuwa na imani kwamba ‘upepo huo mbaya’ ungepita na hali ingekuwa shwari.
Hata hivyo, kadiri siku zinavyozidi kwenda ndivyo hali inavyozidi kuwa mbaya. Kinacholeta wasiwasi zaidi kwa sasa ni kuibuka kwa dalili za ubaguzi wa waziwazi, sambamba na jitihada hatari za kumwaga petroli kwenye moto kwa kuingiza udini kwa nguvu kwenye siasa.
Lakini pasi ‘kuuma maneno’ naomba nielekeze lawama zangu kwa Rais Jakaya Kikwete na chama chake - CCM. Pamoja na wasiwasi uliokuwepo awali, kwamba huenda Rais Kikwete angeendeleza desturi iliyoota mizizi ndani ya CCM kwamba kila wazo lililoanzia vyama vya upinzani (kama hilo la umuhimu wa kuwa na Katiba mpya) ni baya, na hivyo angekwamisha uwezekano wa kupata Katiba mpya, alitushtua wengi alipoonyesha dalili za kuwa amepania kwa dhati kuweka historia kwa kufanikisha suala hilo muhimu.
Mambo yalionekana kwenda vizuri licha ya jitihada za hapa na pale ndani ya CCM kulifanya suala la Katiba mpya kuwa la kiitikadi zaidi kuliko la kitaifa. Wengi mtakumbuka vijembe walivyopigwa baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani walipotaka kukutana na Rais Kikwete. Badala ya kupongeza kile kilichoonekana kama mwanzo mpya wa siasa za maridhiano, baadhi ya wanasiasa huko CCM waliwakebehi wapinzani kuwa wanataka kwenda Ikulu kunywa chai tu!
Dalili za mwanzo kuwa hatma ya suala la Katiba mpya ipo shakani zilianza kujichomoza zaidi baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, chini ya Jaji Joseph Warioba kuweka hadharani Rasimu ya Kwanza ya Katiba mpya, ambapo pendekezo la muundo wa Muungano wa Serikali tatu liliwekwa bayana. Taratibu, CCM, chini ya uongozi wa Kikwete, ilianza harakati za chini chini kujaribu kuingilia mchakato wa Katiba mpya, ikiwa ni pamoja na jitihada za kubinafsisha mchakato huo.
Lakini Mungu si Athumani au John, pamoja na vizingiti vya hapa na pale, hatimaye Rais Kikwete alitangaza majina ya wajumbe 201 kutoka makundi mbalimbali ya jamii, kuingia katika Bunge la Katiba. Lakini kabla ya hapo, tayari Rais Kikwete alishatangaza mkoani Mbeya wakati wa maadhimisho ya kuzaliwa kwa CCM kwamba msimamo wa chama hicho ni Serikali mbili. Japo alitangaza msimamo huo kama Mwenyekiti wa taifa wa CCM, katika mazingira ya kawaida tu, isingewezekana kuwapo kwa mitizamo tofauti kati ya Kikwete wa CCM na Kikwete Rais.
Kuanzia hapo ikawa kama ‘jini lililopo kwenye chupa’ (a genie in the bottle) limefunguliwa. Zikaanza harakati za waziwazi ‘kulazimisha’ matakwa ya chama tawala kwamba muundo wa Muungano lazima ubaki kuwa wa Serikali mbili. Mara zikapatikana taarifa kuwa CCM imetengeneza rasimu yake ya siri.
Mara tu baada ya kikao cha Bunge Maalum la Katiba kuanza, ishara kuwa hali huko mbele inaweza kuwa si shwari zikawa zinajitokeza kila kukicha. Baada ya mshikemshike wa madai ya posho, likaibuka suala la utaratibu wa kupiga kura (yaani kura zipigwe kwa usiri au uwazi.)
Lakini kwa vile tangu awali CCM walionyesha kuwekeza nguvu zao kubwa katika suala la muundo wa Muungano wakitaka Serikali mbili, suala hilo limeteka takriban kila kipengele cha Katiba mpya, na kwa bahati mbaya au makusudi, mjadala wa muundo wa Muungano unazidi kutishia umoja na mshikamano wa taifa letu.
Japo lugha za matusi na kashfa si jambo geni kwenye vikao vya Bunge la Jamhuri, hali imezidi kuwa mbaya kwenye kikao cha Bunge Maalumu la Katiba, tunasikia baadhi ya wajumbe wakiwatuhumu wenzao kuwa mashoga, huko wengine wakienda mbali na kuhoji Uafrika wa wenzao. Lakini kama nilivyobainisha hapo juu kuwa tumeshazoea matusi na lugha chafu bungeni, kuna waliokuwa na imani kuwa “wakimaliza kutukanana, watarejea kwenye suala lililowakutanisha huko Dodoma.”
Mara vikaanza kuibuka vitisho kuwa iwapo Katiba mpya itaridhia Serikali mbili, jeshi litatwaa madaraka. Na aliyeanzisha vitisho hivi si mwingine bali Rais Kikwete katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge hilo la Katiba, wiki chache zilizopita.
Lakini wakati Rais Kikwete aliliongelea suala hilo katika jukwaa la kisiasa (bungeni), mmoja wa wasaidizi wake akaamua kulitoa suala hilo katika anga za siasa na kulipeleka kwenye nyumba za ibada. Hapa ninamzungumzia William Lukuvi.
Inaniwia vigumu kupata maneno stahili ya kumwelezea mwanasiasa huyo ambaye ghafla ametokea kuwa mtu mwenye kauli chafu, hatari na za kiharamia.
Huyu mtu bila aibu wala uoga amediriki kwenda kanisani na kutangaza waziwazi kuwa jeshi litaasi pindi uamuzi wa kuwa na Serikali tatu utakapopitishwa. Naomba nitamke bayana kwamba nahisi Lukuvi ana matatizo kutokana na hatua yake ya kwenda kanisani kufanya mahubiri ya kushawishi jeshi kuasi.
Lakini anayempa jeuri Lukuvi ni Rais Kikwete, kwani naye aligusia suala hilo kwenye hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge la Katiba. Kwa hiyo anachofanya Lukuvi ni kusambaza tu ujumbe ulioanzishwa na Rais Kikwete.
Na wakati Rais Kikwete akiwakemea “wanasiasa wanaomtukana Nyerere na Karume” amekalia kimya matusi ya Lukuvi kwa Mwenyezi Mungu (naam, kutumia nyumba ya ibada kujenga chuki na kuhamasisha uasi wa jeshi ni matusi kwa Mungu.)
Ni watu wenye upeo mdogo tu watakaochukia kusikia kwamba Nyerere na Karume wana mchango katika matatizo tuliyonayo kuhusu Muungano, hasa kwa uamuzi wao wa kulifanya suala hilo kama lao binafsi bila kuangalia madhara yake miaka kadhaa ijayo.
Mara kadhaa Rais Kikwete amekuwa akiasa kuhusu athari za kuchanganya siasa na dini. Amewahi kudai kuwa kuna maadui wa nje wanaotumia suala la dini kwa minajili ya kututenganisha.
Lakini kipi cha kushangaza ilhali kwenye chaguzi kadhaa wamekuwa wakitumia nyumba za ibada kupandikiza chuki dhidi ya wapinzani wao?
Japo hainisumbui sana iwapo Katiba mpya haitopatikana, napata wasiwasi kuona uhuni wa kisiasa (political thuggery) ukihalalishwa kwa kisingizio cha ‘kuhubiri athari za Serikali tatu.’
Lakini nani wa ‘kuokoa jahazi’? Rais Kikwete anakemea wanaowatukana Nyerere na Karume, lakini anapuuza matusi ya wasaidizi wake kwa Jaji Warioba.
Nimalizie makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete kwamba mwakani ataondoka madarakani na kurejea uraiani. Asipotengeneza mazingira mazuri kwake na kwa Watanzania, janga hili linalopikwa na akina Lukuvi litamwathiri naye pia.
Ni muhimu kwa Rais kuweka kando ushabiki wa kisiasa na kuchukua hatua za makusudi kuepusha nchi kutumbukia kwenye machafuko yanayochochewa na mahubiri ya ubaguzi na kuitumia dini kwa minajili ya kisiasa.

Friday, April 18, 2014

Makala yangu Ktk RAIA MWEMA la 16.04.14: "Mafuriko Dar na Kauli za Nyodo za Meya @JerrySilaa"

NIANZE kwa kutoa pole kwa Watanzania kwa janga la mafuriko ambalo linaendelea kusababisha madhara makubwa katika maeneo mbalimbali huko nyumbani.
Japo taarifa zinazosikika zaidi kuhusu mafuriko hayo ni za hali ilivyo Jijini Dar es Salaam, taarifa zinaonyesha kuwa janga hilo linaendelea kusababisha madhara katika sehemu nyingine mbalimbali za nchi yetu.
Kwa vile Taifa bado lipo katika kipindi cha majonzi kufuatia wenzetu kadhaa waliokwishapoteza maisha kutokana na mafuriko hayo, sambamba na maelfu waliopoteza mali zao, inaweza kuwa si wakati mwafaka sana kuanza kunyoosheana vidole. Hata hivyo, kituko kimoja kilichojitokeza mwishoni mwa wiki iliyopita kinaleta haja ya kuwekana sawa wakati tunakabiliana na janga hili.
Jumamosi iliyopita, kulipatikana taarifa iliyoambatana na picha inayomwonyesha Mstahiki Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa, akiwasili mjini Mwanza kwa shughuli za kichama. Ikumbukwe kwamba siku hiyo hali ilikuwa mbaya sana Jijini Dar es Salaam kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa zinazoendelea kuonyesha sehemu mbalimbali huko nyumbani.
Ili kukupa mlolongo sahihi wa matukio, naomba ninukuu kauli husika kuhusiana na tukio hilo. Awali, kutokana na kushangazwa na uwepo wa Meya Silaa jijini Mwanza huku wananchi wake wakikabiliwa na janga la mafuriko, nilibandika picha iliyoambatana na maelezo
Meya wa Ilala Jerry Silaa katika shughuli za kichama muda huu huko Mwanza,” na kuuliza “Mheshimiwa, una taarifa za mafuriko Dar?” Kisha nikaandika tena, “Hawa ndio viongozi wenu. Manispaa ya Ilala ipo katika mafuriko, Meya wa Ilala Jerry Silaa yupo kichama Mwanza.
Baada ya muda mfupi, Meya Silaa alijibu, namnukuu,
Nakuomba radhi kama ungependa niwe Dar nikizuwia mvua isinyeshe.” Kisha akaandika tena “I hate cheap politics (nachukia ‘siasa nyepesi’). Mabonde yote yamejengwa. Mnategemea mito itapumulia wapi? I have remarkable record kwenye rescue missions (nina rekodi ya kupigiwa mfano kwenye jitihada za uokoaji.)” Lakini hakuishia hapo, akaendelea kudai kwamba, “Kwangu wahanga (wa mafuriko) ni kwa wanaoathirika kwa madaraja kukatika iliyosababishwa na watu kujenga mabondeni.” Na katika ‘kuhitimisha’ mjadala huo, Meya Silaa akatoa tuhuma kwamba “Najua viongozi wengi huwa wanaombea watu hata wafe wakabebe jeneza kuonekana wanajali lakini ni unafiki.”
Naomba niweke wazi ya kuwa sina tatizo na Meya Silaa binafsi ila kwa hakika kauli zake zilizosheheni dharau na kiburi zilinikera sana. Na si mimi pekee bali Watanzania kadhaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii pia walishutumu kauli za kiongozi huyo wa Manispaa ya Ilala.
Hata hivyo, pamoja na ushauri wa wengi kwamba hata kama hakuwa na nia mbaya katika kauli hizo basi labda aombe radhi, Mheshimiwa huyo alipuuzia ushauri huo. Mie ni muumini mkubwa wa uhuru wa kujieleza. Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba uhuru pasi nidhamu ni uhuni. Japo kila kiongozi ana uhuru wa kujieleza kama mwananchi yeyote yule, uhuru huo unaambatana na wajibu wa kiongozi husika kwa umma.
Kwa busara za kawaida tu, shughuli za kichama zilizompeleka Meya Silaa huko Mwanza hazikuwa na uzito mkubwa zaidi ya janga la mafuriko Jijini Dar es Salaam ambapo manispaa ya mheshimiwa huyo ilikuwa ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa sana.
Lakini busara zaidi zingeweza kutumika baada ya mheshimiwa kutambua kuwa suala hilo limezua hisia hasi miongoni mwa wananchi, na angeweza kujibu kistaarabu tu, kwa mfano, “ninatarajia kurejea Dar es Salaam  haraka kushirikiana na wananchi wenzangu katika janga hili” badala ya kauli ya kebehi kuwa ‘anaomba radhi kwa anayependa awepo Dar es Salaam  kuzuwia mvua isinyeshe.’
Hivi Rais Jakaya Kikwete alipofanya ziara ya maeneo mbalimbali yaliyoathiriwa na mafuriko hayo alifanya hivyo ili kuzuwia mvua au mafuriko hayo? Na je Makamu wa Rais Dk. Bilal na viongozi wengineo walionusurika katika ajali ya helikopta wakati wakitaka kuanza ukaguzi wa athari za maafa ya mafuriko walitarajia wangezuwia mafuriko hayo?
Ninaamini Meya Silaa anafahamu fika kwamba tunapokwenda kuwajulia hali wagonjwa haimaanishi kuwa tutawaponyesha, tunapokwenda misibani haimaanishi kuwa tutawafufua marehemu. Kumjulia hali mgonjwa au kujumuika msibani ni ustaarabu tuliyojijengea katika mila zetu kuonyesha kuwa TUNAJALI. Na kisaikolojia inaonyesha kuwa mhanga wa tukio lolote lile hupata faraja pindi anapotambua kuwa kuna wanaomjali.
Katika moja ya majibu yangu kwake, nilimfahamisha bayana Meya Silaa kwamba tatizo kubwa la wengi wa viongozi wetu ni kuzowea kusifiwa tu lakini wakikosolewa hukimbilia kudai ni ‘cheap politics.’
Waingereza wanasema “wrong is just that, wrong” (kisicho sahihi kipo hivyo hivyo, hakipo sahihi). Kiongozi kuzipa kipaumbele shughuli za kichama ilhali wananchi wanahangaika na janga la mafuriko si sahihi, na hakuna excuse katika mazingira ya aina hiyo.
Japo Meya Silaa anaweza kuwa sahihi kulaumu ujenzi wa mabondeni kama moja ya sababu zinazochangia mafuriko, lakini kwa hakika mamlaka husika kwa mfano Manispaa ya Ilala inayoongozwa na Meya Silaa zinahusika kwa namna moja au nyingine. Kuwalaumu tu wakazi wa mabondeni hakuwezi kuleta ufumbuzi wa tatizo. Ni muhimu kuelewa kwanini wakazi hao wa mabondeni wanaendelea kuishi maeneo hayo licha ya tishio la mafuriko.
Kwa uelewa wangu, wengi wao ni masikini ambao wanaoishi katika ‘nyumba za mbavu za mbwa’ na ni vigumu mno kwao kumudu kununua ama kujenga nyumba bora katika maeneo salama, achilia mbali huo uwezo wa kununua japo kiwanja.
Lakini eneo jingine ambalo pengine Meya Silaa hawezi kuligusia ni ujenzi unaokiuka taratibu za mipango-miji, unaofanywa na matajiri ambao fedha zao zinawawezesha kupindisha kila aina ya sheria. Wanaoishi mabondeni ni wahanga wanaathiriwa zaidi na kanuni za kiasili za maji kujaa kwenye mabonde, lakini ujenzi holela unaoathiri mfumo wa maji taka ni uingiliaji wa makusudi wa jitihada za binadamu kukabiliana na mafuriko.
Mvua ikinyesha maji yanajaa, na kwa vile mitaro inayopaswa kuyaongoza maji hayo katika maeneo maalumu imezibwa, maji hayo yatamwagikia eneo lolote lile, hata kama si bondeni.
Kuhusu kauli za Meya Silaa, nilimfahamisha kwamba ana bahati ni meya wa manispaa nchini Tanzania kwani laiti angekuwa  meya kwa hapa Uingereza, kisha akaenda mji mwingine kwa shughuli za kichama ilhali wananchi wake wanakabiliana na janga la mafuriko, kungekuwa na uwezekano mkubwa wa harakati za kumng’oa madarakani. Moja ya sifa ya uongozi si tu kujali wananchi bali pia kuonyesha uongozi hasa katika nyakati za majanga.
Kauli hizo zisizopendeza za Meya Silaa zimekuja katika kipindi ambacho Taifa letu lipo katika mchakato wa kupata Katiba mpya. Pengine tukio hili laweza kuwa angalizo muhimu kuhusu Katiba hiyo mpya.
Kwa mfano, je, Katiba hiyo itamwezesha mwananchi wa kawaida kumwajibisha kiongozi ‘mwenye kauli zisizofaa’? Suala hapa si tu katika kauli za kiongozi (iwapo zinafaa au la) bali suala zima la uwajibikaji.
Nimalizie makala hii kwa kurejea kauli ya Rais Jakaya Kikwete wakati alipofanya ziara katika maeneo mbalimbali kuangalia athari za mafuriko, kwamba “mafuriko hayaepukiki na wajibu wa Serikali ni kuwasaidia waathirika.”
Mafuriko kama maji kujaa kutokana na wingi wa mvua hayaepukiki, lakini mafuriko kama ukosefu wa miundombinu bora ya kukabiliana na mafuriko ni suala lililo ndani ya uwezo wetu. Kuna tofauti kati ya mafuriko yanayosababishwa na maji kuvuka kingo za Mto Kilombero huko Ifakara, na mafuriko katika maeneo yasiyo mabondeni jini Dar yanayochangiwa na mfumo duni wa kushughulikia majitaka.
Na japo ninaafikiana na kauli ya Rais kwamba wajibu wa serikali ni kuwasaidia waathirika (sijui ni wapi hao tukirejea kauli ya Meya Silaa) lakini kuna mengi yaliyo ndani ya uwezo wa serikali yanayoweza kupunguza idadi ya waathirika wa majanga kama mafuriko. Kubwa zaidi ni kujijengea uwezo wa kukabiliana na majanga badala ya kusubiri janga litokee ndipo tuanze kutafutana. 

Sunday, April 13, 2014

Sikiza 'nyodo' za Meya Jerry Silaa akihalalisha uwepo wake Mwanza huku wananchi wake wakikabiliana na mafuriko



Huu ni mtizamo wangu, na nilimfahamisha Mstahiki meya Jerry Silaa pia: huyu mtu ana bahati sana kwamba ni Meya wa manispaa nchini Tanzania, ambapo ukisahapata uongozi upo huru kufanya lolote lile- baya au zuri, la busara au la kipuuzi- pasi kuchelea matokeo. Laiti huyu mtu angekuwa Meya wa eneo lolote lile hapa Uingereza, basi Jumatatu angekumbana na wito wa kumtaka aachie ngazi. Ndio, uwepo wake Dar (Ilala) usingezuwia mafuriko, lakini sote twatambua kuwa nyakati za majanga zinahitaji viongozi kuonyesha uongozi kwa dhati (showing leadership). Kilichompeleka Mwanza ni shughuli za kichama, ambazo ninaamini zingeweza kusubiri hadi janga linalowasibu anaowaongoza limeshughulikiwa. 

Japo mwanzoni alileta majibu ya dharau baada ya kusoma 'tweets' hizo mbili za mwanzo hapo juu, lakini akakumbana na hasira za wananchi wengi ambao hawakupendezwa na majibu yake. Lakini kwa vile neno 'samahani' halipo kwenye kamusi za wengi wa viongozi wetu, Mstahiki Meya 'aliingia mitini' kimyakimya...na hajaonekana tena huko twitter hadi wakati ninaposti bandiko hili.

Swali la msingi: Hivi Katiba Mpya tunayohangaika kuipata huko Dodoma itaweza kweli kutengeneza mazingira yatakayowawezesha wananchi kuwashughulikia 'wahuni wa kisiasa' (political thugs)? Jeuri kubwa inayowafanya watawala wetu kufanya (including kusema) chochote ni kutochelea matokeo. Na japo Katiba tuliyo nayo sasa ina sheria nzuri tu za kumpatia mwananchi kile anachostahili (kwa maana ya haki zake), tatizo limebaki katika usimamizi wa sheria hizo, na pengine kubwa zaidi, sheria hizo kubaki kama maandiko tu yasiyoheshimiwa. Je Katiba Mpya (laiti ikipatikana) itaheshimiwa?

Finally, ninaamini Mstahiki Meya Silaa nafsi itamsuta na atakatisha ziara yake huko Mwanza na kuungana na wananchi katika harakati za kukabiliana na athari za mafuriko Dar (kwa yeye ni Manisapaa ya Ilala). See, kwenda kumwona mgonjwa hakumaanishi kutamfanya aopone bali kwaonyesha kuwa flani anajali. Kadhalika, tunapokwenda kwenye misiba haimaanishi kuwa tutamfufua marehemu, lakini ile tu kuwafariji wafiwa kunaonyesha kuwa tunajali. Nam ,Meya Slaa akiwa Illa/Dar hatozuiwa athari za mafuriko (au kama alivyosema mwenyewe "hawezi kzuwia mvua") lakini kibanadamu tu anapaswa kuwa na wahanga wa mafuriko (japo yeye ana-pick and choose nani anastahili kuitwa mhanga).

Saturday, April 12, 2014

Friday, April 11, 2014

Makala yangu ktk RAIA MWEMA Tole la 09/04/14: "Sakata la Muungano- Si kila jambo jema ni sahihi"

KWA familia nyingi huko nyumbani, takriban kila usiku huambatana na kukusanyika mbele ya runinga kuangalia tamthilia mbalimbali.
Hali kama hiyo hujitokeza pia mchana wa mwisho wa wiki ambapo tamthilia hizo hurejewa kwa kujumuisha ‘vipande’ vya wiki nzima.
Nyingi ya tamthilia hizo huwa katika lugha ya kigeni, lakini wengi wa wanaozifuatilia wanamudu kuzielewa bila matatizo. Hata hivyo, yayumkinika kuhisi kwamba hata magwiji wa ufuatiliaji wa tamthilia hizo sasa wanapata wakati mgumu si tu kufuatilia bali hata kuelewa ‘tamthilia’ nyingine ndefu inayoendelea huko Dodoma. Hapa ninamaanisha kikao cha Bunge Maalumu la Katiba.
Pengine ni vema nikawakumbusha wasomaji msimamo wangu kuhusu suala la Katiba mpya, ambao nimeutanabahisha katika makala zangu kadhaa zilizopita.
Kwanza, pamoja na kutambua haja ya kuwa na Katiba bora zaidi ya tuliyonayo sasa, ukweli kwamba matatizo mengi yanayoikabili nchi yetu hayatokani na ukosefu wa sheria bali usimamizi na utekelezaji wake, sioni jinsi Katiba mpya (kama itapatikana) itakavyoweza si tu kuwa ‘mwarobaini’ wa matatizo yetu bali pia kuheshimiwa.
Pili, muundo wa Muungano ndio suala linaloonekana kutawala mjadala wa Katiba mpya, na ninarejea tena kukiri kwamba ninachoona muhimu kwangu si idadi ya serikali zinazounda Muungano- ziwe mbili kama ilivyo sasa, tatu kama ilivyopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, au hata serikali moja kama inavyodaiwa kuwa ndio ‘muundo halisi’ wa Muungano- bali jinsi serikali husika inavyoweza kutimiza majukumu yake na kuwahudumia Watanzania kwa ufanisi.
Kwahiyo basi, kwa lugha nyepesi, msimamo wangu katika suala hili la muundo wa Muungano ni “wowote ule utakaowapatia Watanzania wanachostahili.” Na kwa hakika, malumbano yanayoendelea kuhusu suala hili la muundo wa Muungano yamegubika masuala mengine muhimu yaliyoleta haja ya kuwa na Katiba mpya.
Sasa, kwa vile mazingira yanaashiria kwamba kupatikana au kutopatikana kwa Katiba mpya kunategemea muafaka katika suala hilo la muundo wa Muungano, basi hata sie ‘tusiolitilia maanani sana’ tunalazimika kulijadili kwa marefu na mapana. Hiki ni kikwazo ambacho bila kukivuka chaweza kuondoa uwezekano wa kupatikana Katiba mpya.
Mwanzoni mwa makala hii, nimefananisha kikao cha Bunge Maalumu la Katiba na tamthilia. Lakini kichekesho ni kwamba wakati tamthilia nyingi za kigeni zinazotawala kwenye runinga za huko nyumbani zinaeleweka licha ya kuwa katika lugha za kigeni, hii ya Bunge la Katiba si tu inazidi kutoeleweka bali inapoteza ladha kila kukicha.
Hakuna haja ya kurejea mlolongo wa matukio yaliyokwishakujitokeza katika Bunge hilo, hasa kwa vile takriban yote yanakera; kuanzia madai ya nyongeza ya posho hadi Bunge hilo kugeuka ulingo wa kuonyeshana umahiri wa vijembe na lugha zisizopendeza.
Lakini sasa kuna suala jipya ambalo si tu linazidisha ugumu wa mjadala wa muundo wa Muungano bali pia linatishia hata uhai wa Muungano wenyewe. Suala hili ni nyaraka mbalimbali za kuthibitisha uhalali/uhalisia wa Muungano.
Ningependa kukiri kwamba sielewi nyaraka hizo za Muungano ni ngapi, lakini ninachofahamu ni kwamba moja ni hiyo inayofahamika kama Hati ya Muungano. Sasa, katika mazingira yanayoweza tu kuonekana katika filamu ya kutisha (horror movie), sahihi ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere inaonyesha dalili ya ‘kuchakachuliwa.’ Mlolongo wa maswali unaibuka hapo: je, sahihi hiyo imechakachuliwa au hati nzima imechakachuliwa na ndiyo maana sahihi inazua utata? Nani aliyefanya ‘uhuni’ huo? Na kubwa zaidi, kwa nini?
Lakini ukidhani kizaazaa pekee ni katika suala hilo la sahihi ya Nyerere tu, basi subiri mpaka utakapofahamu kwamba madai kuwa Hati ya Muungano ambayo awali ilidaiwa ipo Umoja wa Mataifa (UN) nayo yana walakini baada ya UN kudai haina hati hiyo. Swali jingine, iko wapi? Kwa nini ilidaiwa ipo UN ilhali si kweli? Nani huyo anayedanganya? Kwa nini?
Kabla ya kuandika makala hii nimekutana na maelezo ya mchambuzi mmoja kwenye mtandao mmoja wa kijamii akieleza kwamba kwa uelewa wake, hati iliyowasilishwa katika Bunge Maalumu la Katiba huko Dodoma, na yenye sahihi za Nyerere na Pius Msekwa sio ‘Hati ya Muungano’ (Articles of the Union) bali ni Sheria ya Muungano (the Act of the Union) iliyotungwa na Bunge wakati huo kupitisha Articles of the Union, na kusainiwa na Nyerere na Msekwa (kama Katibu wa Bunge wakati huo).
Na hata hati hiyo ingekuwa ndio Hati halisi ya Muungano, bado kuna tatizo jingine la sahihi za Nyerere na Msekwa kuwa na walakini. Kadhalika, inaelezwa kwamba hati hiyo imeongezwa maneno ‘kwa kompyuta’ japo kila mwenye uelewa anafahamu kwamba kompyuta hazikuwapo nchini katika miaka hiyo ya 1960.
Mchambuzi huyo anahitimisha kwamba hati ‘zilizotoweka’ ni nakala halisi ya Serikali ya Tanganyika, nakala halisi ya SMZ, nakala halisi ya Bunge la Tanganyika, nakala halisi ya Baraza La Wawakilishi, nakala halisi ya Mwanasheria Mkuu, nakala halisi ya Nyerere, na nakala halisi ya Karume.
Maswali kadhaa yanajitokeza, ikiwa ni pamoja na, je nakala hizo ‘zimetoweka’ kweli au hazijawahi kuwapo? Nani anahusika na kutoweka huko? Kwa nini? Na maswali mengine lukuki.
Vilevile, gazeti moja la Kiingereza la huko nyumbani, katika toleo lake la juzi, liliripoti kwamba aliyekuwa Katibu wa kwanza wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Salum Rashid, alieleza kwamba Mzee Karume hakuwahi kusaini hati yoyote kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Utata huo unaogubika uhalali na/au uhalisia wa Muungano umenifanya kuhisi kwamba kuna mtu/watu fulani mahala fulani anadanganya/wanadanganya. Swali: ni nani? Na kwa nini anadanganya/wanadanganya?
Niliwahi kuandika katika moja ya makala zangu huko nyuma kwamba pamoja na nia nzuri ya kuunganisha Tanganyika na Zanzibar, Nyerere na Karume walikosea kufanya suala hilo kama la ‘wao binafsi’ na si la Watanganyika na Wazanzibari wote.
Pamoja na dhamira zao nzuri, sidhani kama viongozi hao waliangalia mbali zaidi ya ajenda ya umoja na mshikamano, hivyo kutotilia maanani uwezekano wa matatizo ya kisheria au hata ridhaa ya wananchi huko mbele. Na, binafsi naona mapungufu haya kama moja ya vyanzo vikuu vya matatizo ya Muungano.
Lakini pengine badala ya kuwalaumu waasisi hao wa Muungano ni muhimu kutambua mazingira ya kisiasa ya wakati huo. Hicho kilikuwa kipindi cha kujenga Taifa, huku mfumo wa kisiasa ukiwa hauruhusu mawazo tofauti na ya watawala. Hivi tumeshawahi kujiuliza wazo la kuunganisha Tanganyika na Zanzibar lilikuwa la kidemokrasia kiasi gani, kwa maana ya kusaka ridhaa ya wadau halisi wa Muungano huo, yaani Watanganyika na Wazanzibari?
Kwa bahati mbaya (au kwa makusudi), kwa kiasi kikubwa chama tawala CCM kinataka kurejea kosa hilohilo lililopelekea kuzaliwa Muungano ‘wenye matatizo.’ Wanataka kulazimisha matakwa yao ya muundo wa Muungano wa serikali mbili. Kuna busara moja inafundisha hivi, “Si kila tendo jema ni sahihi. Kwa mfano, kumpa chakula ‘kigumu’ mtu mwenye njaa ni tendo zuri, lakini kumpa chakula kingi kigumu mtu mwenye njaa kali ni hatari kwani inaweza kumfanya mtu huyo kuvimbiwa na hata kupoteza maisha.”
Dhamira ya CCM kutaka kunusuru muundo wa sasa wa Muungano (wa serikali mbili) inaweza kuwa nzuri. Lakini kulazimisha dhamira hiyo (pasi kujali uzuri wake) ni jambo hatari. Na hata kama CCM walitaka kulazimisha dhamira yao hiyo basi angalau wangejiandaa vya kutosha badala ya kukurupuka, na sasa tunashuhudia matatizo mengine makubwa zaidi yanayozua utata wa Muungano mzima wanaotaka kuinusuru.
Nihitimishe kwa kuishauri CCM na wote wanaotaka kulazimisha muundo wa Muungano wa serikali mbili, kwamba suluhu pekee ni kwa suala hilo kupelekwa kwa wananchi ili hatimaye waamue kuhusu muundo wa Muungano wanaotaka. Na si tu kulipeleka suala hilo kwa wananchi bali pia kutowatisha kwa minajili ya kuwalazimisha wafuate matakwa ya chama hicho tawala.
Ni ushauri mwepesi lakini kila anayeijua CCM anafahamu kuwa ni chama ‘kisichoshaurika’ wala ‘kuambilika.’ Kwao, wapo tayari Watanzania wakose Katiba mpya iwapo dhamira ya chama hicho kung’ang’ania muundo wa Muungano wa serikali mbili itakwama.
Kama ambavyo hata tukipata Katiba mpya inaweza kutokuwa na manufaa pasipo nia ya dhati kuiheshimu na kuitekeleza kwa ufanisi, pasipo nia ya dhati ya kusaka muafaka katika suala la muundo wa Muungano na hatma ya Katiba mpya kwa ujumla, kikao cha Bunge Maalumu la Katiba kitaishia kuwa tamthilia ambayo si tu inakera bali pia ya gharama kubwa kwa wananchi.
PENYE NIA PANA NJIA

Saturday, April 05, 2014

Ishu ya Muungano: Kuna mtu mahala flani anadanganya. Swali ni kwanini?


Kimsingi, mchakato wa kupata Katiba mpya umegeuka kuwa hukumu ya Muungano wa 'Tanganyika' (Tanzania Bara) na Zanzibar. Mengi yamesahongelewas na nisingependa kuyarudia hapa, lakini suala jipya lililojitokeza ni sahihi za Marehemu Baba wa Taifa na Marehemu Karume.

Kuna taarifa kwamba baadhi ya nyaraka hazina sahihi ya Marehemu Karume, hali inayoweza kuashiria kuwa uamuzi wa Muungano ulifanywa na Nyerere pekee. Japo historia inaeleza tofauti, kwa kawaida, hati ya mkataba huwa na angalau na sahihi za wahusika wawili au zaidi kutegemea mazingira ya mkataba husika.

Lakini hata hiyo sahihi ya Nyerere yenyewe imezua utata. So far, kuna sahihi mbili (yawezekana zipo nyingine). Lakini sio tu sahihi kuwa zaidi ya moja, katika moja ya nyaraka za Muungano kuna maneno yameongezwa. Maelezo yanayotolewa ni kuwa kompyuta ilitumika...bila hata kuuliza kompyuta ilitumika kwa malengo gani, swali la msingi ni je Tanzania- au Tanganyika ilikuwa na kompyuta mwaka 1964?

Licha ya sahihi ya Nyerere, kuna taarifa pia ikwamba hata sahihi ya Katibu wa Bunge wa wakati huo, Pius Msekwa nayo ina walakini. 

Mara kadhaa katika maandiko yangu nimebainisha kuwa haileti maana kujadili muundo wa Muungano pasipo wajjumbe wa Bunge la Katiba kupatiwa nyaraka muhimu zinazohusu Muungano huo. Maelezo yaliyotolewa na wahusika ni kwamba eti kuna nakala moja tu ya moja ya nyaraka muhimu za Muungano, kwahiyo haiwezi kupelekwa Dodoma kwa kuhofia inaweza kupotea. Huu sio utoto tu bali ni ubabaishaji wa hali ya juu. Kwanini wahusika wasichapishe nakala kisha kuzi-certify as true copies of the original?

Anyway, hebu analia katika picha ya hapo juu kuhusu ipi ni sahihi halisi ya Mwalimu Nyerere.

Nihitimishe bandiko hili kwa kuyumkinisha kuwa utata unaojitokeza kuhusu nayaraka muhimu za Muungano unaashiria kwamba kuna mtu flani mahala flani anaongopa (someone somewhere is lying). Tusichojua ni kwanini?

TIME WILL TELL 

Magazeti ya Tanzania Leo Jumamosi Apr 5,2014: Katiba Mpya katika hatihati ya kupatikana

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

 
Design by Free WordPress Themes | Bloggerized by Lasantha - Premium Blogger Themes | Hot Sonakshi Sinha, Car Price in India