Featured Posts

Showing posts with label Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015. Show all posts
Showing posts with label Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015. Show all posts

Saturday, March 24, 2012

Zitto Kabwe: "Ndio,Nataka Kuwa Rais..."

Photo 

Ndio nataka kuwa rais

Kwanza niseme wazi kabisa kabisa kuwa Urais ninautaka.
Ninaamini ninao uwezo wa kuwa Rais. Ninaamini nina uzalendo wa kutosha na utashi wa kuleta mabadiliko stahili wa namna nchi yetu inavyoongozwa. Ninajua kuwa nchi yetu imesahau maendeleo ya watu na kujikita katika maendeleo ya vitu. Ninajua kuwa hivi sasa viongozi wetu wengi wanaangalia zaidi mitindo (styles) badala ya mambo ya msingi (content). Ninajua kuwa maendeleo vijijini yamesahaulika. Ninajua nchi yetu inahitaji Uongozi wa kufanya mabadiliko makubwa (transformation) badala ya mabadiliko ya juu juu (cosmetic change). Ninajua ‘transformation’ inahitaji maamuzi magumu yatakayoudhi wengi na hasa mabwana wakubwa wa nchi za magharibi mfano kuzuia nchi yetu kuuza malighafi tu. Ninajua rushwa, ufisadi na ubadhirifu wa Mali ya Umma ni kikwazo kikubwa cha maendeleo yetu na kwamba lazima hatua madhubuti zichukuliwe kuzuia na kutokomeza ufisadi. Ninajua rasilimali kama Madini, Mafuta na Gesi, Ardhi n.k. ni lazima zifaidishe wananchi wa nchi yetu.
Hivyo, nchi inahitaji Kiongozi wa juu atakayekabili changamoto hizi. Ninaamini ninaweza kuwaongoza Watanzania wenzangu kukabili changamoto hizi. Sio kazi rahisi lakini ni kazi ambayo lazima Mtanzania mmoja aifanye. Mimi nataka kuifanya. Nina uwezo wa kuifanya.
Hata hivyo kazi hii hata kama naitaka ni lazima wenye nchi waamue kunipa kazi hii. Ni lazima kwanza Chama changu kiseme wewe ndio mwanachama unaestahili kuifanya kazi hii. Ni lazima Watanzania wengi waseme wewe ndio mwananchi mwenzetu unayeweza kuchukua jukumu hili. Kuitaka tu haitoshi. Ni lazima wananchi wakuamini na kukupa jukumu hili.
Sasa kama wananchi watasema huyu Zitto anapaswa kubeba jukumu hili mwaka 2015 tuache iwe. Kama watasema hapana wewe bado mpaka mwaka 2020 au hata 2025 tuache iwe hivyo. Pia Kama hawataki kabisa tuache iwe hivyo.
Mjadala wa umri wa kugombea Urais imekuwa mjadala mkali sasa. Mjadala huu baadhi ya watu kwa sababu wanazojua wao wameamua kuita ni mjadala wa Zitto na January. Kwamba ni mjadala unaobagua Wazee. Mjadala unaopandikiza chuki na sumu za kibaguzi. Kwamba ni mjadala wa Kitabaka na kuwa Zitto na January sio tabaka stahili la vijana walio wengi. Sitamsemea January, nitajibu baadhi ya hoja za mwandishi wa makala mojawapo kama Zitto. January akitaka atamjibu naye kivyake.
Mwandishi anasema yeye hapingi hoja ya umri, bali anapinga aina ya watu wanaoshadidia hoja hiyo. Anaipenda hoja ila hapendi watoa hoja. Hoja nzuri lakini Zitto na January wabaya. Amelisema hilo mwanzo kabisa wa makala yake. Kwa hiyo kwake yeye hoja ingeletwa na vijana wengine asingekuwa na shida wala isingekuwa hoja hatari. Kwa kuwa hoja imeletwa na Zitto na January (ingawa sisi sio waanzilishi wa hoja hii) ni hoja ya kibaguzi. Nawashangaa sana wasomi wa siku hizi. Wasomi wanaojadili watu badala ya masuala.
Mwandishi anasema kwamba vyama vya siasa haviandai vijana kuwa viongozi. Nitamweleza.
Chama changu kinalea na kukuza vijana kuwa viongozi. Mimi binafsi nimejiunga na chama changu nikiwa na umri wa miaka 16, mtoto. Nimekulia ndani ya chama. Nimepewa majukumu ya kawaida kabisa ya chama kama kusimika miti ya bendera, kupokea viongozi na kuandaa mikutano. Nikiwa Chuo Kikuu Mwenyekiti wa sasa wa Chadema ndugu Mbowe alikuja kuniomba sasa nishiriki kikamilifu kukijenga upya chama. Yeye alikuwa Mbunge wa Hai akitaka chama kiwe imara zaidi, akaambiwa kuna mwanachama wenu kule Mlimani. Wakati huo CHADEMA kilikuwa chama ambacho watu wanakikimbia isipokuwa watu wa Kigoma na Kilimanjaro, Shinyanga, Karatu na Ukerewe. Vijana walikuwa wanajipambanua na CCM zaidi ama CUF au TLP kuliko hiki chama cha mabwanyenye. Huu ni mwaka 2001, muongo mmoja tu uliopita. Mimi na Freeman Mbowe ndio tumefanya mabadiliko yote yanayoonekana CHADEMA. Tumeingiza watu wapya, tumeandika Katiba upya. Ilipofika mwaka 2005 tukasema Freeman Mbowe nenda kwenye Urais, tulijuwa tunashindwa lakini tulitaka kujenga chama chetu. Tukapata Wabunge. Wabunge Wakafanya kazi. Tukaingia mwaka 2010 katika uchaguzi kama chama imara tunachokwenda kuchukua dola.
Katika mchakato huu tukaingiza vijana kwenye chama na kuwalea. John Mnyika hakuwa CHADEMA, tena alikuwa mgumu sana kuingia kwenye chama chetu. Tukampa moyo. Tukampa majukumu. Leo ni mmoja wa rasilimali watu kubwa sana katika siasa za nchi yetu. Halima Mdee hakuwa mwanasiasa kabisa. Tukampa moyo. Tukampa majukumu. Leo ni Mbunge mahiri kabisa.
Baadhi ya watu wazima waliingia CHADEMA kufuata vijana. Vijana tulifyeka pori kwanza. Nani anasema hatulei vijana kuwa viongozi wazuri? Nani haoni hazina ya viongozi vijana hivi sasa ndani ya Bunge kutoka vyama vyote? Kuna namna bora ya kulea viongozi zaidi ya kuwapa majukumu?
Mbowe alikuwa ananifuata pale Hall 1, tunakwenda kufanya kazi za chama usiku kucha, kusoma na kuchambua makabrasha ya kisera na mikakati. Ninarudi chuo usiku wa manane wakati wanafunzi wengine ama wapo wanajisomea au wamelala. Kazi ya kujenga taasisi inayoitwa chama cha siasa.
Lakini kujengwa kuwa kiongozi sio kazi ya chama pekee. Ni kazi ya jamii kwa ujumla. Wakati wanafunzi wenzangu walikuwa wanaomba kufanya kazi za mafunzo kwenye taasisi kubwa Kama Benki Kuu, nikiwa mwaka wa pili Chuo Kikuu nilikwenda kufanya internship TGNP. Kujifunza Bajeti ya kijinsia na kuipa hoja za kiuchumi. Kina mama wa TGNP wakanijenga na kunipika kiuongozi.
Chuo Kikuu sikuwa nasoma Sosholojia, lakini rafiki yangu mkubwa alikuwa Chachage. Sikuwa nasoma lugha, lakini mshauri wangu alikuwa Lwaitama. Sikuwa nasoma sheria lakini nilikuwa namwakilisha Shivji na kusoma mada zake alizopasa kuwakilisha kwenye semina kadhaa kuhusu haki za binadamu. Nimefunzwa na makundi ya watu mbalimbali na sio chama changu pekee. Jamii ndio yenye jukumu la kufunda vijana kuwa viongozi. Jamii inafanya kazi hiyo?
Inasemwa mjadala huu ni hatari kwa namna ulivyopenyezwa. Kupenyezwa? Huu mjadala wa umri umeanza kuzungumzwa mimi nikiwa nipo Chuo Kikuu. Vijana kupitia National Youth Forum Kama Taasisi ya vijana wamekuwa wakisema jambo hili toka miaka ya katikati ya tisini. Jukwaa hili la Vijana chini ya viongozi wake kina Hebron Mwakagenda wamekuwa wakitoa Maazimio na Maazimio kwamba umri wa kugombea Urais upo juu sana toka miaka ya tisini. Taasisi ya TYVA imekuwa ikijenga hoja hii toka miaka ya 2000. Hii sio hoja mpya hata kidogo. Hoja hii haijapenyezwa. Hii ni hoja ya vijana ya miaka mingi sana. Lakini sishangai kuona inaonekana ni hoja mpya kwani watanzania uwezo wetu wa kutunza kumbukumbu ni mdogo sana. Pia tunapenda kujadili mtoa hoja na sio hoja yenyewe. Mfuatiliaji yeyote makini wa siasa za vijana wa Tanzania kupitia makongamano ya vijana anajua hii sio hoja iliyopenyezwa na Zitto au January. Kuijadili kwa kumwangalia Zitto na January ni kuchoka kufikiri.
Hoja hii haina hatari yeyote inayosemwa na mwandishi. Hoja hii ni hoja kama hoja nyingine yeyote na inaweza kupita au kukataliwa. Hii sio hoja ya watu fulani. Ni hoja ya vijana ya siku nyingi sana. Vijana hawa wanajiona kupitia vijana wengine walio kwenye nafasi mbalimbali kisiasa au hata katika sekta binafsi. Mfano vijana wa Kigoma ninakotoka wakiniangalia wanajiona. Ndio wanaona tuko sawa. Wanaona mimi ni mwenzao. Nimekua miongoni mwao. Nimesoma nao. Nimecheza nao. Nimehangaika nao. Wanaona Ubunge nilionao ni Dhamana tu na hawanizungumzishi kama mtu kutoka tabaka fulani, bali kama mwenzao.
Ninaishi maisha ninayoishi. Siishi Manzese kwa Mfuga Mbwa. Siishi Masaki pia. Naishi Tabata, kwenye nyumba ya kupanga. Tabata wanaishi vijana wote wale wa tabaka la chini kama asemalo mwandishi na pia tabaka la kati na labda tabaka la juu. Najua na kusikia machungu ya vijana wasio na ajira na ndio maana nahangaika kwa kutumia nafasi ya Ubunge kujaribu kuisukuma Serikali iweke sera zinazotekelezeka za kutatua tatizo la ajira kwa vijana. Ndio maana nahangaika kila siku kujenga hoja kwamba Serikali iingilie kati ukuaji wa uchumi ili pia wanyonge wafaidike. Ninasikia machungu ya vijana wasio na ajira maana ndio walionipigia kura kuwa Mbunge. Zaidi ya hayo nakutana nao sana kuzungumza namna ya kusaidiana.
Nakutana nao mitaani kwa mijini na vijijini ninakokwenda kila wakati. Nakutana nao kwenye mitandao ya kijamii, wananiandikia na mimi ninawajibu. Nagawana nao kidogo nilichonacho ili nao waweze kijikwamua. Nawasaidia vijana wenye vipaji kukuza vipawa vyao na kupata kipato. Mwandishi anapata wapi haki ya kusema sentensi rahisi rahisi kwamba mimi sisikii machungu ya vijana wenzangu?
Ninashinda na vijana wa aina zote, ndio kazi kubwa ya Mwakilishi anayefanya kazi yake. Nina marafiki wavuvi, mafundi seremala, waimbaji wa Bongo Flava, machinga na hata wasio na ajira. Nina marafiki wenye makampuni yao, wafanyakazi wa mashirika ya Umma, wasomi wa Vyuo Vikuu na wafanyabiashara wakubwa. Mwakilishi yeyote wa wananchi lazima asikie machungu ya jamii nzima vinginevyo hatoshi.
Kijana mwenye umri wangu ana mambo mengi anayofanana nami. Ana mambo mengi ya kujifunza kutoka kwangu. Hapa katikati ilikuwa ni kama jambo lisilowezekana kijana wa aina yangu kutoka familia masikini kabisa kuwa Mbunge. Baada ya Zitto kuwa Mbunge na kutokana na kazi niliyofanya Bungeni katika Bunge la Tisa, vijana wengi walihamasika na kusema wanaweza. Leo tuna vijana wadogo kabisa kutoka familia za kawaida kabisa ni Wabunge na wanafanya vizuri. Kina Kafulila, kina Mkosamali, kina Silinde hawa ni watoto wa kimasikinj kabisa ambao ni wa kwanza kupata shahada kwenye familia zao. Hii ni nguvu ya ‘inspiration’ kutoka kwa rika linalofanana. Sugu ni mkubwa kwangu kiumri, lakini kuingia kwake siasa kumechangiwa sana na kazi zangu pamoja na wenzangu kwenye Bunge.
Kuna vijana wengi zaidi nchini kwetu wanasema ninataka niwe kama Zitto, kama January, kama Halima Mdee. Tunazungumza nao. Tunaishi nao. Ni ndugu zetu. Ni rafiki zetu. Tunaishi nao mtaani. Tunakwenda nao kwa kinyozi mmoja. Tunakwenda muziki pamoja. Ninajua machungu ya vijana. Ninafanyia kazi machungu ya vijana. Ndio kazi yangu ya kila siku kama Mbunge, kama Mwakilishi wao.
Mwandishi anasema mjadala unalenga kuleta ubaguzi. Sioni hoja yake. Wanaosema umri wa kugombea Urais ushushwe chini ya miaka 40 hawasemi wazee wasigombee. Wanasema tupanue wigo wa haki hii ya kugombea. Wanaozungumza ubaguzi ndio wenye kupenyeza mbegu za kibaguzi. Kwa kuwa wanawaza kibaguzibaguzi basi kila jambo huliangalia kibaguzi. Kama Katiba inasema yeyote mwenye haki ya kupiga kura ana haki ya kugombea nafasi yeyote ya uongozi, ubaguzi unatoka wapi? Hoja zote zinazotolewa na mtoa hoja kuhusu ubaguzi zinasambaza mbegu ya ubaguzi.
Mwandishi sasa anawaambia Watanzania waanze kufikiri sasa zamu ya nani. Mimi binafsi sijawahi kusema hii ni zamu ya vijana. Ila nimesema changamoto za sasa za nchi zinahitaji mtu mwenye uwezo wa kuzikabili, ninaamini mtu huyo ni kijana. Ninaamini kuwa kila kizazi kina ajenda zake. Kizazi chetu kina kazi ya kuhakikisha uhuru wa kiuchumi wa nchi yetu. Kizazi cha kina Mwalimu kilikuwa cha ukombozi na kujenga Taifa moja. Mwandishi hamwamini Frantz Fanon?
Hoja ya kwamba mjadala huu unataka kununua hisia za wanyonge ni hoja isiyo na [mashiko] kabisa. Mimi nimechaguliwa na wanyonge mara mbili kuwa Mbunge wao. Wanyonge wamenipa Ubunge bila kutoa rushwa. Wamenipa Ubunge kwa kuniamini. Sasa kwa nini sasa ninunue hisia zao? Hii hoja ina misingi gani? Hii ni hoja ya kubandika. Hii ni hoja ya kubumba maneno ili mwandishi aonekane kwamba anafanya uchunguzi wa kitabaka. Hakuna dhana ya tabaka katika hoja hii kama ilivyo kuwa hakuna dhana ya tabaka kwa wazee au hata wanawake. Hoja hii haizuii kwa namna yeyote ile wananchi kuhoji chanzo cha ufukara wao. Kwanza wanaosemwa kwenye hoja hii ndio wapo mstari wa mbele kuhakikisha Mali ya Nchi inatumika wa maendeleo ya wananchi. Mimi binafsi nimeanzisha mjadala wa rasilimali Madini nchini mpaka kutungwa kwa sheria mpya inayoweka misingi ya nchi kufaidika na Madini. Mimi binafsi na wenzangu tumekuwa mstari wa mbele kuhakikisha serikali inatekeleza sheria mpya.
Mwandishi amesahau Buzwagi? Mwandishi amesahau hoja ya Mkonge inayotaka wanyonge wapewe mashamba ya Mkonge na wawezeshwe na Serikali kulima Katani? Mwandishi amesahau hoja ya kusimamia sekta ya nyumba ili wanyonge wasinyonywe na wenye nyumba ambayo imetolewa na mmoja wa wanaotetea hoja ya umri kushushwa? Ama mwandishi ana wanyonge wake anaowasemea? Sio hawa manamba kwenye Mkonge. Sio hawa vijana wachimbaji wadogo. Sio hawa vijana wanaoshindwa kulipa kodi ya nyumba mwaka mzima? Wanyonge wa mwandishi ni wanazuoni wanaoishi kwa fedha za walipa kodi ambao hawana shida ya kujiuliza kama watakula au watalala maana Serikali au wafadhili wa masomo yao wanawalipia malazi na chakula. Kama wanyonge wake ni hawa waliotupigia kura sisi ili kuwawakilisha Bungeni, basi mwandishi hajui asemalo.
Hoja ya umri wa kugombea Urais, kwa kuweka pa kuanzia ama kuweka kikomo inapaswa kujadiliwa bila kuangalia majina ya wanaotetea hoja hii. Ijadiliwe kwa faida na hasara zake. Kujenga hoja kwa misingi ya kitabaka ni kuchochea ubaguzi na kunyweshea mbegu za kibaguzi. Nani ana uhakika kuwa Zitto atakuwa anaishi ifikapo mwaka 2015? Kwamba tusiandike Katiba yenye kupanua wigo wa kutoa haki ya kugombea Urais kwa sababu ya Zitto?
Huu woga dhidi ya Zitto unatoka wapi?
CHANZO:Zitto na Demokrasia

Sunday, October 09, 2011

Changamoto Zinazoikabili CCM Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015


Tuipende,tuichukie lakini ukweli unabaki kuwa CCM ndio chama tawala.Kwa mantiki hiyo kila Mtanzania,including sie tusiokuwa wananchama wa chama chochote kile cha siasa tunalazimika kuwa na interest na hali ya mambo ndani ya chama hicho.Afterall,tofauti zetu za kiitikadi hazimaanishi uadui kama unavyohubiriwa na akina Nape.Sote ni Watanzania,na iwe CCM,Chadema,CUF,nk vyote ni vyombo tu vya kutushirikisha katika siasa za nchi yetu kwa namna moja au nyingine.

Anyway,niende kwenye mada.CCM inakabiliwa na changamoto kubwa katika kumpata mgombea wake anayetarajiwa kumrithi Rais Jakaya Kikwete atakapomaliza muda wake mwaka 2015.Naomba kuorodhesha changamoto hizo kama ifuatavyo

MGOMBEA KUTOKA ZANZIBAR

Japo Katiba ya Jamhuri ya Muungano na ile ya CCM hailazimishi utamaduni usio rasmi wa kupokezana nafasi ya mgombea urais kati ya CCM Bara na Zanzibar,yayumkinika kuamini kuwa baada ya miaka 20 (1995-2015) ya CCM Zanzibar kutotoa mgombea kwenye nafasi ya Urais wa Muungano upande huo utakuwa unatarajia kuwa sasa ni zamu yao.Baada ya Rais Mzanzibari Ali Hassan Mwinyi,alikuja M-Bara Benjamin Mkapa aliyetawala kwa miaka 10 kabla ya kurithiwa na M-Bara mwingine Jakaya Kikwete ambaye kufikia mwaka 2015 atakuwa ametawala kwa miaka 10.

Kwa vile katika utamaduni mwingine usio rasmi ndani ya CCM mgombea atakayepitishwa mwaka 2015 (na ikitokea akashinda) anaweza kuwa madarakani kwa miaka 10 (kwa maana kuwa anatarajiwa kupitishwa tena mwaka 2020-kama ilivyokuwa kwa Mwinyi,Mkapa na sasa Kikwete), Wazanzibari wakikubali mgombea ajaye wa CCM atoke Bara itamaanisha wakose nafasi kwa miaka 30 mfululizo.

Tofauti na ccm Bara ambapo uongozi wake una sauti kuliko wanachama,kwa Zanzibar wanachama na viongozi wa kawaida wana influence kubwa ndani ya chama hicho.Wakati uongozi wa CCM Zanzibar unaweza kuridhia mgombea ajaye ataoke Bara,ni vigumu kuhisi wanachama na viongozi wa kawaida wakakubali miaka mingine 10 pasipo Mzanzibari mwenzao kushika urais kupitia CCM.

Iwapo CCM Bara watashinikiza lazima mgombea atoke Bara basi Wazanzinari wanaweza kutumia turufu ya "tunatoka nje ya Muungano" na hili linaweza kuzua sokomoko kubwa.

MGOMBEA/RAIS MUISLAM KISHA MKRISTO (na vice versa)

Utamaduni mwingine ndani ya CCM ni kuzungusha nafasi ya urais (au mgombea wa urais) kati ya Waislam na Wakristo.Baada ya miaka kadhaa ya utawala wa Mwalimu Nyerere ikaja zamu ya Muislam Mwinyi,ambaye naye alirithiwa na Mkristo Mkapa,kabla ya ujio wa Muislam Kikwete.Katika mambo ambayo CCM inapaswa sifa nyingi ni pamoja na umakini wake katika kudili na ishu nyeti ya dini (japo wanasiasa mufilisi wameanza kutumia udini kwa minajili ya kusaka mafaniko yao binafsi kisiasa).Chama hicho kimejitahidi sana kuzingatia ukweli wa mgawanyo wa kiimani miongoni mwa Watanzania ambapo Waislam na Wakristo wanatengeneza takriban robo mbili za wakazi wote wa nchi yetu (robo nyingine ni wanaofuata imani nyingine pamoja na wapagani)..

Sasa,kwa kuzingatia ukweli kuwa Kikwete ni Muislam,inatarajiwa mgombea urais wa CCM mwaka 2015 awe Mkristo ili kudumisha utamaduni huo usio rasmi.Iwapo mgombea huyo atatoka Bara,haitokuwa vigumu kumpata.Tatizo ni iwapo mgombea atatakiwa kutoka Zanzibar.Kama tujuavyo,takriban asilimia 99 ya Wazanzibari ni Waislam,na hali ni kama hiyo kwenye uongozi wa CCM visiwani humo.Uwezekano wa kumpata mgombea urais kutoka Zanzibar ambaye ni Mkristo ni mgumu pengine kuliko uwezekano wa Gaddafi kuwa mgombea urais wa Marekani kuchuana na Rais Barack Obama hapo mwakani.

Kwa mantiki hiyo,kama changamoto ya kwanza itapatiwa ufumbuzi,yaani CCM kufanikiwa kupata mgombea wake kutoka Zanzibar,tatizo litabaki kwenye changamoto ya pili,yaani kupata mgombea Mkristo kutoka visiwani humo.

CHAGUO LA KIKWETE

Ni wazi Rais Kikwete angependa kupata mrithi atakayeweza kumpa amani baada ya kustaafu.Baada ya kuonjesha ladha ya 'ujeuri' pale baadhi ya vigogo wa chama hicho wanapodaiwa kutaka kumng'oa kwenye kiti cha uenyekiti wa chama hicho kwa kigezo cha kutenganisha kofia ya urais na uenyekiti wa CCM,yayumkinika kuamini kuwa asipokuwa makini kumpata mrithi atakayehakikisha anakula pensheni yake bila usumbufu wala hofu ya kukumbana na yaliyomkuta Chiluba...

Lakini Kikwete kulazimisha chaguo lake kutategemea namna atakavyoweza kumpromoti kuanzia sasa.Wachambuzi wengi wa siasa zetu wanafahamu kuwa Kikwete hana sauti kubwa ndani ya chama hicho.Kimsingi,mtu kama Edward Lowassa ana nguvu takriban mara mbili ya alizonazo Kikwete ndani ya chama hicho.Nguvu pekee ya mwenyekiti huyo ni kutoka kwa watu wa Idara ya Usalama wa Taifa ambao licha ya kumpatia dossiers zenye "machafu" ya viongozi wenzie wa CCM,pia wanaweza kulazimisha matakwa ya Kikwete yakatimia kwa mbinu chafu za kiintelijensia.Hilo linafanyika sehemu nyingi tu duniani ambapo siasa na intelijensia zimefunga ndoa isiyo rasmi.

Lakini hili la mashushushu kuingilia siasa za ndani ya CCM linategemea zaidi siasa za ndani za Idara ya Usalama wa Taifa.Wajuzi wa mambo wanafahamu mgogoro wa chini chini ndani ya Idara hiyo kuelekea mchakato wa CCM kumpata mgombea wake mwaka 2005.Tofauti za kimaslahi miongoni mwa viongozi waandamizi wa Idara hiyo zilitishia kwa kiasi kikubwa jina la Kikwete kupitishwa,na hata alipofanikiwa kupitishwa na hatimaye kushinda urais baadhi ya viongozi waandamizi wa Idara hiyo walijikuta majeruhi.

LOWASSA NA 'PIGA UA' YAKE

Mpende au mchukie, lakini Edward Lowassa ameendelea kuwa mwanasiasa mwenye nguvu na ushawishi mkubwa ndani na nje ya CCM.Licha ya uwezo wake mkubwa wa kifedha,Lowassa amewasaidia viongozi wengi wa CCM kuwepo madarakani,iwe kwa misaada ya kifedha au kimkakati.

Japo hajaweka msimamo wake hadharani,wachunguzi wengi wa siasa wanaamini kuwa ndoto za mwanasiasa huyo kumrithi Kikwete bado zipo hai.Inaaminika kuwa chanzo cha ndoto hizo ni mkataba usio rasmi kuwa Kikwete angemwachia Lowassa jahazi la kuongoza Tanzania baada ya kumaliza miaka yake 10 ya Urais.Mahesabu yalikwenda vizuri hadi pale ilipoibuka skandali ya Richmond iliyopelekea Lowassa kuachia ngazi.Laiti hilo lisingetokea basi muda huu wala nisingeandika makala hii kwa vile ingekuwa wazi kuwa Lowassa ndiye Rais ajaye baada ya Kikwete.

Kinachomsaidia Lowassa ni jinsi anavyotumia kila nafasi ipasavyo kuhakikisha jina lake linaendelea kuwa masikioni mwa Watanzania.Mwanasiasa huyo yupo radhi hata kuwaunga mono wanasiasa wa vyama vya upinzani alimradi kufanya hivyo kunamweka karibu zaidi na wapiga kura.

Kadhalika,pamoja na kuhusishwa na ufisadi,Lowassa anakubalika kama mtu anayemudu kufanya anachoamini,jambo linalomtofautisha na Rais Kikwete ambaye anaelemewa zaidi na kutaka kuwafurahisha watu wake wa karibu.Lowassa yupo tayari aonekane mbaya ndani ya CCM lakini aishie kuonekana mkombozi kwa Watanzania.

Na katika kumtendea haki,Lowassa ana 'u-Sokoine' wa namna flani.Hasiti kutoa maamuzi na anaweza kusimamia maamuzi yake.Laiti mwanasiasa huyu asingekuwa na mawaa ya ufisadi basi Tanzania ingeweza kupata carbon copy ya Sokoine.

Kuna wanaomwona Lowassa kama mwanasiasa anayeweza kubadilika kwa sababu kuu mbili.Kwanza,utajiri mkubwa alionao unaweza kabisa kumshawishi asitumie madaraka yake kuendeleza utaratibu wa kuifanya Tanzania kuwa shamba la bibi.Japo utajiri sio kigezo cha fisadi kutotamani fedha zaidi lakini madaraka kama ya Urais yanaweza kumfanya mtu apate huruma kwa anaowaongoza.Kikwete ana huruma lakini tatizo ni kwamba huruma yake kwa mafisadi ni kubwa ziadi ya ile aliyonayo kwa walalahoi.Hilo halina mjdala na mwenyewe anajua hilo.

Kingine kinachoweza kumpa faida Lowassa ni network yake ambayo inaweza kabisa kupenya Zanzibar kuwashawishi wamuunge mkono.Ukichanganya na advantage nyingine kwamba yeye ni Mkristo (ambayo inamfanya awe eligible kwa mujibu wa changamoto ya pili hapo juu),

Lakini pengine faida nyingine aliyonayo mwanasiasa huyu ni ukaribu wake na Idara ya Usalama wa Taifa,ambayo penda usipende itacheza nafasi muhimu kwa mgombea mwana-CCM yeyote anayetaka kumrithi Kikwete.Japo sina hakika kwa sasa ukaribu huo upo katika hali gani lakini unaweza kuwa na faida kubwa kwake.

Kubwa zaidi ya yote ni ukweli kwamba Lowaasa anamfahamu Kikwete in and out.Kwa mantiki hiyo,anaweza kumwandama Kikwete hata atakapomaliza muda wake wa Urais.Na kwa vile by then Kikwete hatokuwa na nguvu za kutosha ukilinganisha na hali ilivyo sasa ambapo yeye ni mkuu wa nchi, yayumkinika kuamini kuwa angependa kuwa na maadui wachache wenye nguvu na uwezo wa kumwangamiza.Kikwete anaweza kujikuta anakabiliwa na mzimu uleule ambao yeye na wanamtandao wenzake walimsababishia Rais Mkapa.

Inafahamika kuwa Kikwete na timu yake waliweka wazi kwa Mkapa kuwa laiti asingepitishwa basi aidha angegombea (na pengine kushinda) kupitia tiketi ya chama cha upinzani.Sasa ukizingatia Kikwete hakuwa karibu kihivyo na vyama vya upinzani kwa wakati huo,ukaribu wa Lowasaa kwa wapinzani unaweza kulifanya tishio la aina hiyo kuchukuliwa kwa uzito mkubwa.Ikumbukwe kuwa nafuu pekee kwa Kikwete atakapostaafu ni kwa CCM kubaki madarakani kwani kuna kila dalili kuwa kama chama cha upinzani kikishinda basi anaweza kabisa kupandishwa kizimbani kujibu tuhuma lukuki za ufisadi.

Je CCM wanawezaje kukabiliana na changamoto hizi?Moja ya njia mwafaka ni kujaribu kuiga utaratibu wa siasa za uchaguzi nchini Marekani ambapo wananchama wenye nia ya kuwania kupitishwa kugombea urais wanatangaza dhamira zao mapema.Pamoja na faida ya kumfanya mwanachama mwenye dhamira hiyo kufahamika vema kwa wapiga kura,utaratibu huo unaambatana na hatari zake.Kwa mwananchama kujitambulisha hadharani mapema anaweza kuwapatia maadui zake wa kisiasa ammunition ya kutosha kumteketeza mapema,na ikifika wakati wa kupiga kura za kumpitisha mgombea anaweza kuwa amekwisha kabisa.

Anyway,kwa leo naomba kuishia hapa.Nitaendelea na mada hii wakati mwingine

 
Design by Free WordPress Themes | Bloggerized by Lasantha - Premium Blogger Themes | Hot Sonakshi Sinha, Car Price in India